Dar es Salaam. Upande wa utetezi katika kesi ya uhujumu uchumi inayowakabili Mkurugenzi wa Uthaminishaji Almasi na Vito Tanzania (Tansort) Archard Kalugendo na wenzake umeutaka upande wa mashtaka wafanye jitihada za kukamilisha upelelezi.
Pamoja na Kalugendo wengine ni Mthamini wa Madini ya Almasi wa Serikali, Edward Rweyemamu ambao ni watumishi kutoka wizara ya madini
Hatua hiyo imekuja baada ya upande wa mashtaka kudai mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu wa Mahakama ya Kisutu, Huruma Shaidi leo Jumatatu Juni 3, 2019 kuwa jalada lipo kwa Mkurugenzi wa Mashtaka (DPP) na upelelezi upo kwenye hatua za mwisho hivyo mahakama hiyo ipange tarehe nyingine.
Wakili wa utetezi Hassan Kiangio amedai shauri hilo lipo mahakamani kwa zaidi ya miaka miwili hivyo upande wa mashtaka wafanye jitihada za kukamilisha upelelezi.
"Imeshapita miaka miwili sasa washtakiwa wapo ndani, tunataka upande wa mashtaka kuharakisha upelelezi ili shauri liweze kwenda mbele zaidi," amedai Kiangio.
Baada ya maelezo hayo, Hakimu Shaidi ameahirisha shauri hilo hadi Juni 14, 2019 itakapokuja kwa ajili ya kutajwa.
Pia Soma
- Serikali ya Tanzania yatoa sababu nne ya deni la Taifa kuongezeka
- Rungwe ahojiwa polisi, aachiwa kwa kufanya mkutano wa ndani
- Pongezi ya Nape kwa Waziri Makamba yaibua mjadala
Kalugendo na Rweyema kwa mara ya kwanza walifikishwa Mahakamani hapo, Septemba 15, 2017, wakikabiliwa na shitaka moja la kuisababishia Serikali hasara ya Sh 2.4 bilioni
Katika hati ya mashitaka, washitakiwa hao wanadaiwa kutenda kosa hilo Agosti 25 na 31, 2017 katika maeneo mbalimbali ya Jiji la Dar es Salaam na Mkoa wa Shinyanga.
Kwa pamoja wakiwa wathaminishaji wa Almasi wa Serikali na waajiriwa wa wizara ya Nishati na Madini, waliisababishia Serikali hasara ya Dola za Marekani 1,118,291.43 ambazo ni sawa na Sh 2.4 bilioni.