Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

VIDEO: Watano mbaroni kwa kughushi na kujipatia mamilioni, akiwemo ofisa wa Magereza

Video Archive
Fri, 17 Aug 2018 Chanzo: mwananchi.co.tz

Pwani.  Watu watano wakiwemo watumishi wanne wa Hazina ndogo Kibaha wanashikiliwa na polisi mkoani Pwani kwa tuhuma za kughushi nyaraka mbalimbali za malipo na kuiba Sh284.8milioni ambazo ni fedha za Serikali.

Watuhumiwa hao wanadaiwa kutenda kosa hilo kati ya Aprili na Mei, 2018, walishirikiana na ofisa mmoja wa Jeshi la Magereza mkoani humo.

Akizungumza leo Ijumaa Agosti 17, 2018 kamanda wa polisi mkoani Pwani, Jonathan Shanna amesema watuhumiwa hao waliiba fedha hizo kwa vielelezo zinazoonyesha zililipwa mzabuni wa kampuni ya Lukozi na Usambara Grocery and Vegetable Supplies ya mkoani humo.

Shanna amewataja watuhumiwa hao Stanley Kansabala, (45), mkazi wa Kigamboni Dar es salaam, Boaz Lyimo (31), mkazi wa Kimara, Imani Kilembe (43), mkazi wa Suka ambaye yeye katika upekuzi anadaiwa kukutwa na Sh4.6milioni nyumbani kwake na Hallo Ntambi (38) aliyekutwa na Sh 4.2milioni nyumbani kwake, wote wakiwa ni wahasibu wa Hazina ndogo.

Mwingine ni ofisa wa Jeshi la Magereza mkoani hapa anayeshughulika na kazi za uhasibu SP Komango Makala (53)  mkazi wa Magereza Kibaha na wote watafikishwa mahakamani wakati wowote uchunguzi utakapokamilika.

Amesema pia wamemnasa mkurugenzi wa kampuni hiyo ya Lukola na Usambara, Omary Singano kwa mahojiano zaidi kwa kuwa kampuni hiyo ndiyo imeingiziwa fedha hizo, hivyo amemtaka kutii sheria bila shuruti kwa kufika ofisi ya mkuu wa upelelezi Pwani mara moja.

Katika tukio jingine , hakimu wa mahakama ya wilaya ya Bagamoyo ambaye jina lake linahifadhiwa amekamatwa kwa tuhuma za kushirikiana na matapeli wauzaji wa viwanja  na mashamba kusaini hati mbalimbali katika tarehe tofauti kisha kijipatia Sh18 milioni kutoka kwa ofisa wa Jeshi la Wananchi (JWTZ) kwa njia ya utapeli.

“Hakimu huyu amekuwa akisaini hati mbalimbali zinazotumiwa na matapeli kujiingizia kipato kwa kuwauzia watu eneo moja la ardhi kwa mara mbili,” amesema.

“Anawagongea muhuri wa Serikali anaweka sahihi yake kuwezesha utapeli huu na katika uthibitisho amesaini hati moja ya umiliki ya nyumba na kujipatia Sh18milioni kutoka kwa afisa wa JWTZ.”

Chanzo: mwananchi.co.tz