Dar es Salaam. Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu imepanga Februari 21, 2019 kumsomea maelezo ya awali mlimbwende wa Tanzania mwaka 2006, Wema Sepetu.
Hatua hiyo inatokana na upelelezi wa shauri hilo kukamilika na hivyo upande wa mashtaka kuiomba mahakama hiyo ipange tarehe kwa ajili ya kumsomea mshtakiwa maelezo hayo.
Wema anakabiliwa na shtaka moja la kuchapisha video ya ngono na kusambaza katika mitandaoni ya kijamii.
Leo Jumatano Februari 13, 2019 mwanasheria wa Serikali, Glori Mwenda ameieleza mahakama hiyo mbele ya Hakimu Mkazi, Maira Kasonda wakati kesi hiyo ilipokuja kwa ajili ya kutajwa.
"Shauri lilikuja kwa ajili ya kutajwa na taarifa njema ni kwamba upelelezi wa shauri hili umekamilika, hivyo tunaomba tarehe kwa ajili ya kumsomea maelezo ya awali, mshtakiwa huyu" amedai Mwenda.
Hakimu Kasonde baada ya kusikiliza maelezo hayo, ameahirisha kesi hiyo hadi Februari 21, 2019.
Wema ambaye anatetewa na wakili, Ruben Simwanza, alifikishwa kwa mara ya kwanza Kisutu Novemba Mosi, 2018 kujibu shtaka hilo. Wema yupo nje kwa dhamana.
Katika kesi ya msingi, Wema anadaiwa Oktoba 15, 2018 katika maeneo mbalimbali ya jiji la Dar es Salaam alichapisha video ya ngono na kuisambaza katika mtandao wake wa kijamii wa Instagram.
Soma Zaidi: Mahakama yahoji upelelezi kesi ya Wema kutokamilika