Dodoma. Waziri wa Fedha na Mipango, Dk Philip Mpango amesema watu saba wamekamatwa na kufikishwa mahakamani kwa kuhusika na biashara haramu ya kubadilisha fedha za kigeni.
Dk Mpango aliyeongozana na Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT) Profesa Florens Luoga ameyasema hayo leo Jumatatu Aprili Mosi, 2019 katika mkutano wake na waandishi wa habari jijini Dodoma.
Amesema Serikali inatoa tahadhari kwa wananchi kutoshiriki kwenye biashara ya kubadilisha fedha za kigeni kwa njia zisizo halali.
“Hivi sasa kuna taarifa kuwa baadhi ya maeneo ya mipakani na majiji ya Dar es Salaam na Arusha wamejitokeza watu wanaofanya biashara haramu ya kubadilisha fedha za kigeni ambao wamewaathiri baadhi ya wananchi kwa wizi,” amesema.
Amesema vyombo vya usalama ikiwemo jeshi la polisi vimeongeza nguvu katika kuhakikisha biashara haramu (Black Market) inatokomezwa na hivi sasa wahalifu saba wamekamatwa na kufikishwa mahakamani.