Dar es Salaam. Mwandishi wa Habari za Uchunguzi, Erick Kabendera amepandishwa kizimbani katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Dar es Salaam nchini Tanzania na kusomewa mashtaka matatu ikiwamo la utakatishaji fedha.
Kabendera amefikishwa mahakamani hapo leo Jumatatu Agosti 5, 2019 ambapo amesomewa mashtaka hayo mbele ya Hakimu Mkazi Mwandamizi, Agustino Rwezile.
Mashtaka yanayomkabili Kabendera ni kupanga na kushiriki mtandao wa uhalifu, kukwepa kodi zaidi ya Sh173 milioni na utakatishaji fedha zaidi ya Sh173 milioni.
Upande wa mashtaka umesema upelelezi bado haujakamilika hivyo Hakimu Rwezile ameiahirisha kesi hiyo hadi Agosti 19, 2019 itakapokuja kwa ajili ya kutajwa.
Kutokana na mashtaka hayo, upande wa utetezi, umeyaondoa maombi ya dhamana yaliyokuwa yameyawasilishwa mahakamani hapo kutokana na kesi iliyofunguliwa na Serikali ya Tanzania dhidi ya mwandishi huyo wa habari kutokuwa na dhamana.
Kabendera amepandishwa mahakamani ikiwa ni siku ya saba tangu alipokamatwa na Polisi wa Tanzania Julai 29 mwaka 2019 akiwa nyumbani kwake Mbweni, Dar es Salaam nchini Tanzania.
Habari zinazohusiana na hii
- Uhamiaji Tanzania yachukua paspoti saba nyumbani kwa Kabendera
- Mwandishi wa habari Tanzania achukuliwa kwa nguvu nyumbani kwake, polisi wakana
- Wakili aibua mapya kushikiliwa kwa Kabendera
Mambosasa alisema walimkamata Kabendera baada ya kupelekewa wito wa kufika polisi lakini akakaidi.