Moshi. Zoezi la kuteketeza vielelezo vilivyotumika kama ushahidi katika kesi ya mauaji ya mwanafunzi wa shule ya Scolastica, Humphrey Makundi(16) imegonga mwamba baada ya mawakili wa utetezi kutaka wateja wao kuwepo.
Wakati akitoa hukumu ya kesi hiyo Juni 3, 2019, Jaji wa Mahakama Kuu, Firmin Matogolo aliagiza vielelezo hivyo, panga lililotumika katika mauaji hayo na nguo za marehemu kuteketezwa.
Vielelezo vingine vilikuwa ni simu za washtakiwa walizotumia kuwasiliana usiku na kuitana eneo la tukio, ambazo jaji huyo aliamuru zitaifishwe na Serikali.
Awali, akiwasilisha ombi la kusitisha kazi hiyo mbele ya naibu msajili wa mahakama hiyo, wakili Elikunda Kipoko ameeleza umuhimu wa wateja wake kuwepo, kwamba baadhi yao wameshakata rufaa.
"Suala la kuchoma vielelezo hivi haliwezi kufanyika bila wateja wetu kuwepo, hapa inatakiwa umakini kwa sababu zoezi ili lifanyike lazima wateja wetu wawepo,” amedai wakili Kipoko.
Hata hivyo, wakili wa Serikali Lucy Kyusa aliyekuwa akisikiliza kesi hiyo alieleza kuwa zoezi hilo lipo kisheria kutokana na amri iliyotolewa na mahakama.
Pia Soma
- Mapato ya forodha mpaka wa Namanga yafikia Sh54 bilioni
- Mikataba ya ajira za madereva mbioni kuanza nchini Tanzania
- Kauli ya Membe kuhusu Lissu yaibua mjadala mtandaoni
June 3, 2019 mahakama hiyo ilimhukumu kunyongwa hadi kufa aliyekuwa mlinzi wa shule hiyo, Hamis Chacha ,huku mmiliki wa shule hiyo, Edward Shayo pamoja na aliyekuwa mwalimu wa nidhamu, Laban Nabiswa wakihukumiwa kifungo cha miaka minne jela kila mmoja kwa kuficha ukweli wa mauaji ya mwanafunzi huyo.
Novemba 6, 2017 mwanafunzi huyo aliuawa na kisha mwili wake kutupwa katika mto Ghona mita 300 kutoka ilipo shule hiyo.