Dar es Salaam. Upelelezi wa kesi ya kukutwa na vipande 18 vya meno ya tembo vyenye thamani ya Sh171.7milioni mali ya Serikali ya Tanzania inayowakabili washtakiwa watano bado haujakamilika.
Washtakiwa hao wanaokabiliwa na mashtaka manne katika kesi ya uhujumu uchumi ni mfanyabiashara mkazi wa Kigamboni, Salehe Majaliwa (31) na Mwanaisha Ndwangila(36) mkazi wa Tunduma.
Wengine ni Sauda Athuman (36) mkazi wa Mbagala, Hamisi Ulega (27) na Abdallah Mohamed (38) wote wakazi wa Lindi.
Leo Alhamisi Desemba 27, 2018 wakili wa Serikali, Amina Kombakono ameieleza Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu mbele ya hakimu mkazi mkuu, Salum Ally kuwa upelelezi wa shauri hilo haujakamilika, kuiomba mahakama kupanga tarehe nyingine ya kutajwa.
Baada ya kusikiliza maelezo hayo hakimu Ally ameahirisha kesi hiyo hadi Januari 8, 2019 huku washtakiwa wakirejeshwa rumande kutokana na kesi hiyo kutokuwa na dhamana.
Washtakiwa hao walifikishwa mahakamani hapo kwa mara ya kwanza Desemba 12, 2018.
Inadaiwa kuwa kati ya Novemba Mosi na Novemba 21, 2018, katika Mkoa wa Dar es Salaam na Lindi, kwa pamoja walishiriki kuuza nyara za Serikali ambazo ni vipande 18 vya meno ya tembo, vyenye thamani ya dola za Marekani 75,000 sawa na Sh171.7milioni bila kuwa na kibali kutoka kwa mkurugenzi wa Wanyamapori.
Katika shtaka la pili, ambalo pia ni kuongoza mtandao wa uhalifu, linalowakabili Mwanaisha na Mohamed, inadaiwa siku hiyo na eneo hilo, washtakiwa hao walitoa fedha kiasi cha Sh 171.7milioni ambazo zilisaidia kununua vipande 18 vya meno ya tembo.
Katika shtaka la tatu, ambalo ni kukutwa na meno ya tembo linalomkabili Majaliwa pekee, inadaiwa kuwa Novemba 21, 2018 katika eneo la Buza Wilaya ya Temeke, mshtakiwa alikutwa na vipande hivyo vya meno ya tembo.
Katika shtaka la nne, ambalo ni kujihusisha na biashara ya meno ya tembo, linalowakabili washtakiwa wote, inadaiwa kuwa kati ya Novemba Mosi na Novemba 21, 2018, washtakiwa hao walisafirisha vipande 18 vya meno ya tembo kutoka Lindi kuja Dar es Salaam, bila kuwa na kibali.