Dar es Salaam. Wakili wa Serikali mwandamizi, Wankyo Simon amedai kesi ya utakatishaji fedha inayomkabili aliyekuwa meneja wa Benki ya Wanawake Tanzania (TWB) tawi la Mkwepu, Priscus Shirima ipo kwenye hatua ya mwisho kukamilika.
Shirima, mfanyabiashara na mkazi wa Dodoma Area D anakabiliwa na mashtaka matatu, likiwemo la utakatishaji fedha katika kesi ya uhujumu uchumi namba 95/2018.
Simon amedai mbele ya hakimu mfawidhi wa mahakama ya Kisutu, Kelvin Mhina kuwa kesi hiyo lilikuja kwa ajili ya kutajwa na wapo katika hatua za mwisho kukamilisha upelelezi.
"Shauri lilikuja kwa ajili ya kutajwa na nimeshawajulisha upande wa utetezi kuna vitu vichache vinakamilishwa," amedai Simon.
Simon baada ya kueleza hayo, wakili wa utetezi, Gaudensia Mdaki ameutaka upande wa mashtaka kuhakikisha wanakamilisha upelelezi kwa wakati kwa kuwa shauri hilo ni la muda mrefu.
Shirima amefikishwa kwa mara ya kwanza katika Mahakama ya Kisutu Desemba 13, 2018 kujibu mashtaka hayo.
Pia Soma
- Upande wa utetezi kutumia video kumhoji shahidi kesi ya kina Mbowe
- Makonda ataka usafi Dar kuendelea kama ilivyokuwa katika mkutano Sadc
- Ripoti yawataja wenye ualbino kuishi kwa wasiwasi kuelekea uchaguzi
Anadaiwa kutenda kosa hilo Juni 20, 2016 katika benki hiyo kwa kufanya muamala wa uongo kwa kuhamisha Sh120 milioni kutoka akaunti namba 0310137001 ya Florah Lyatuu kwenda akaunti yake namba 0380073121.
Katika shtaka la pili, siku na eneo hilo akiwa kama meneja wa tawi hilo aliiba Sh120 milioni.
Katika shtaka la utakatishaji, Shirima anadaiwa kutenda kosa hilo kati ya Juni 2016, katika benki hiyo.
Siku hiyo mshtakiwa alijihusisha na muamala wa Sh120 milioni kwa kuruhusu na kufanya malipo kutoka akaunti namba 0380073121 na kuilipa kampuni ya Sekorizi Ltd kupitia hundi tatu zenye namba 000127, 648806 na 1648791, huku akijua kuwa fedha hizo si halali.