Dar es Salaam. Upande wa utetezi katika kesi ya uhujumu uchumi inayomkabili mfanyabiashara, Abdul Nsembo maarufu Abdulkandida na mkewe, Shamim Mwasha umeomba upande wa mashtaka kuhakikisha unakamilisha upelelezi kwa wakati ili kesi hiyo iweze kuendelea na hatua nyingine.
Nsembo na Shamim wakabiliwa na shtaka la kusafirisha dawa za kulevya aina ya heroin.
Wakili wa utetezi, Hajra Mungula na Charles Kisoka wametoa ombi hilo leo Jumatatu Mei 27, 2019 katika mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu wakati kesi hiyo ilipokuja kwa ajili ya kutajwa.
Ombi hilo limetolewa mbele ya Hakimu Mkazi Mfawidhi, Kelvin Mhina baada ya upande wa mashtaka kudai kuwa upelelezi wa kesi hiyo bado haujakamilika.
“Kwa kuwa kesi hii haina dhamana na wateja wetu wanaendelea kusota rumande tunaomba upande wa mashtaka wajitahidi kukamilisha upelelezi kwa wakati ili kesi hii iweze kuendelea kwa hatua nyingine " amedai Kisoka.
Awali, wakili wa Serikali, Simon Wankyo amedai shauri hilo lilikuja kwa ajili ya kutajwa na upelelezi wa kesi hiyo bado haujakamilika.
Pia Soma
- MADAI: DPP awatuhumu wabunge kwa rushwa, Spika ajibu
- Utalii wa utamaduni washika kasi Japan
- Kesi washitakiwa wa meno ya tembo ya Sh1.466 bilioni Juni 11 na 12
- Watoto 20 kuzibuliwa mishipa na kuzibwa matundu ya moyo kwa Cath Lab
Kwa mujibu wa hati ya mashtaka, wawili hao wanakabiliwa na kesi ya uhujumu uchumi namba 36/2019.
Wanadaiwa kwa kusafirisha dawa za kulevya aina ya Heroin zenye uzito wa gramu 232.70 wakati wakijua kufanya hivyo ni kosa kisheria.
Wanadaiwa kutenda kosa hilo Mei Mosi, 2019 katika eneo la Mbezi Beach jijini Dar es Salaam.
Kwa mara ya kwanza washtakiwa hao walifikishwa Kisutu Mei 13, 2019.