Dar es Salaam. Upelelezi wa kesi inayomkabili aliyekuwa Mkurugenzi wa Mipango na Ufuatiliaji na Tathmini wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa(Takukuru), Kulthum Mansoor bado haujakamilika.
Mshtakiwa huyo anakabiliwa na mashtaka nane likiwemo la utakatishaji wa fedha kiasi cha Sh1.477,243,000.
Wakili wa Serikali, Tully Helela aliieleza Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu leo Alhamisi Mei 23, 2019 kuwa shauri hilo kilikuja kwa ajili ya kutajwa akieleza kuwa upelelezi bado unaendelea na kuomba kupangiwa tarehe nyingine.
Pia Soma
- VIDEO: Ndugai, mbunge Masele watuhumiana bungeni
- Mwanamke aua jambazi kwa kisu
- Zao la utomvu laiingizia Saohill Sh700 milioni
- VIDEO: Bunge la Tanzania lamsamehe Masele
Katika kesi ya msingi mshtakiwa anadaiwa kughushi tarehe tofauti Januari 2013 na Mei 2018 akiwa makao makuu ya Takukuru iliyopo jijini Dar es Salaam alitoa barua ya ofa ikionyesha barua hiyo imetoka katika halmashauri ya Bagamoyo huku akifahamu kufanya hivyo ni kosa la kisheria.
Kosa jingine katika tarehe tofauti kati ya Januari 2012 na Mei 2017 akiwa Upanga mshtakiwa alijipatia fedha kwa njia ya udanganyifu Sh5.2 milioni kutoka kwa mtumishi wa Takukuru, Alex Mavika kama malipo ya kiwanja kilichopo kijiji cha Ukuni wilayani Bagamoyo huku akionyesha yeye ni mmiliki wakati akijua ni uongo.
Katika kosa la utakatishaji wa fedha kati ya tarehe tofauti Januari 2013 na Mei 2018 akiwa eneo la Upanga jijini Dar es Salaam mshtakiwa alijipatia Sh1.477,243,000 huku akijua fedha hizo ni zao la makosa mengine.