Dar es Salaam. Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu imekubali ombi la upande wa mashtaka la kutaka kukutana na mwandishi wa habari wa Tanzania, Erick Kabendera kwa ajili ya kukamilisha majadiliano ya kumaliza kesi yake.
Kabendera anakabiliwa na mashtaka matatu likiwemo la kutakatisha Sh173 milioni.
Uamuzi huo umetolewa leo Jumanne Februari 11, 2020 na Hakimu Mkazi Mkuu wa Mahakamani hiyo, Janeth Mtega baada ya upande mashtaka kuwasilisha ombi hilo.
Wakili wa Serikali Mkuu, Faraja Nchimbi amewasilisha ha ombi hilo na kuiomba mahakama hiyo iruhusu upande wa mashtaka kukutana na mshtakiwa huyo kwa ajili ya kukamilisha majadiliano ya mwisho ya kumaliza kesi hiyo.
Kesi hiyo imeahirishwa hadi Februari 17, 2020.
Januari 27, 2020 kesi hiyo ilipotajwa mahakamani hapo, wakili wa Serikali, Gloria Mwenda aliieleza mahakama hiyo kuwa majadiliano kati ya ofisi ya mkurugenzi wa mashtaka (DPP) na Kabendera yalikuwa yakiendelea.
Habari zinazohusiana na hii
- Wakili asema Kabendera bado anajadiliana na DPP
- Erick Kabendera amuomba msamaha Rais
- Kabendera bado anajadiliana na DPP
- Mahakama yamzuia Erick Kabendera kwenda kumuaga mama yake
Katika shtaka la kwanza anadaiwa katika kipindi hicho, alijihusisha na mtandao wa uhalifu kwa kutoa msaada kwa genge la uhalifu kwa nia ya kujipatia faida.
Shtaka la pili anadaiwa katika kipindi hicho bila ya sababu alikwepa kodi ya Sh173.2 milioni aliyotakiwa kulipa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA).
Katika shtaka la tatu, anadaiwa kutakatisha Sh173.2 milioni huku akijua fedha hizo ni mazalia ya kosa la kujihusisha na genge la uhalifu na utakatishaji fedha.
Endelea kufuatilia Mwananchi kwa taarifa zaidi.