Zanzibar. Mkazi wa kijiji cha Makunduchi mkoani Kusini Unguja, Zuwena Haji Mwadini (14) amefariki kwa kujinyonga kwa kutumia mtandio.
Kamanda wa polisi mkoa wa Kusini Unguja, Suleiman Hassan Suleiman alisema kwamba tukio hilo lilitokea Agosti 17.
Alisema binti huyo alikuwa mwanafunzi wa darasa la sita na kwamba, sababu za kujinyonga ni ugomvi baina yake na mdogo wake.
Suleiman alisema tofati baina ya watoto hao ilisababisha kuchukua uamuzi huo na kuongeza kuwa tukio hilo si la kawaida.
Pia, Suleiman aliwataka vijana kuacha kuchukua uamuzi wa haraka.
Naye mkurugenzi wa Chama cha Waandishi wa Habari Wanawake Tanzania (Tamwa) Zanzibar, Dk Mzuri Issa alisema wazazi na walezi wahakikishe wanakuwa karibu na watoto wao.
“Wazazi ikitokea wakashindwa kufuatilia mienendo ya watoto wao basi lolote linaweza kutokea pindi watoto wanapotofautiana, ni bora kuwa karibu nao,” alisema.
Naye kamishna mstaafu wa Tume ya Haki za Binadamu Tanzania kwa upande wa Zanzibar, Mohamed Khamis alisema kuna haja ya kutolewa elimu kwa jamii ili vijana wasijiingize kwenye uamuzi usio sahihi ikiwamo kujiua.