Dar es Salaam. Baada ya kusambaa kipande cha video kinachoonyesha askari watatu wa Kikosi cha Usalama Barabarani wakimshambulia dereva wa lori mkoani Songwe, Kamanda wa Polisi wa mkoa huo, Mathias Nyange amesema watatoa taarifa za tukio hilo.
Tukio hilo lililotokea katika mkoa wa Songwe liliibua hisia na kushangaza watu wengi kutokana na jinsi askari hao walivyokuwa wakitumia nguvu kumkamata dereva huyo ambaye haikufahamika mara moja alikuwa akitokea au kuelekea wapi na kwa kosa gani.
Baada ya kuonekana kuzidiwa nguvu askari mmoja alimng’ata dereva huyo shingoni jambo lililomfanya apige kelele za kuomba msaada.
Akizungumza na Mwananchi leo Jumapili Januari 13, 2019, Nyange amesema japokuwa yuko likizo lakini anaamini waliopo wamejipanga kutoa taarifa kamili ya tukio hilo haraka iwezekanavyo.
“Mimi mambo yote huwa yanatolewa ofisini kwa njia ya mikutano na waandishi wa habari, si kwa njia ya simu hivyo mtafahamu ni kitu gani,” alisema Nyange.