Tabora. Watu tisa wanashikiliwa na Jeshi la Polisi mkoani Tabora kwa tuhuma za kuiba na kununua mali za wizi.
Akizungumza leo Jumanne Mei 28, 2019 Kamanda wa Polisi Mkoa wa Tabora, Emmanuel Nley amesema watuhumiwa hao wamekamatwa baada ya kutolewa taarifa na wasamaria wema kutoka maeneo mbalimbali.
Amebainisha kuwa polisi wamefanya msako kuanzia Mei 17, 2019 na kufanikiwa kupatikana kwa mali mbalimbali kutoka kwa watuhumiwa hao aliodai kuwa wamekiri kuhusika katika matukio hayo.
Pamoja na kukutwa na baadhi ya mali za wizi, pia wamekutwa na silaha zinazodhaniwa kutumiwa katika uhalifu.
Ametaja baadhi ya silaha kuwa ni nondo, visu, mapanga, nyundo, misumeno na bisibisi.
Baadhi ya mali walizokamatwa nazo watuhumiwa ni pamoja na subwoofer tano, runinga tano, redio, saa za ukutani, vitenge na mabegi.
Pia Soma
- Askofu azikwa na mamia, aacha watoto 18 wajukuu 12
- Handeni wazindua binti shujaa
- Alichokisema Nyalandu baada ya kuachiwa kwa dhamana
Wanaoshikiliwa ni Hassan Jumanne, Shaban Masudi, Musa Said, Ramadhan Adam, Shaban Karume, Omary Ngoloko, Seif Hussein, Yusufu Magili na Karume Ramadhani.
Amewataka wananchi kwenda kituo kikuu cha Polisi kuangalia kama mali hizo ni zao.