Bukoba. Polisi Mkoa wa Kagera linawashikilia watu tisa kwa tuhuma za mauaji ya watoto wawili wa familia moja.
Watoto hao Auson Respikius (7) na Alistidia Respikius (5) walichinjwa na miili yao kutupwa kichakani katika kijiji cha Mashule wilayani Bukoba, Mkoa wa Kagera, ikiwa ni baada ya kupotea Jumapili, Oktoba 21,2018 na miili yao kupatikana jana.
Kaimu Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kagera, Izack Msengi amesema watuhumiwa hao wamekamatwa kwa ajili ya hatua za uchunguzi.
Msengi amesema familia iliyopoteza watoto, kwa nyakati tofauti iliwahi kuchomewa nyumba na wananchi kwa tuhuma za uchawi wakishinikiza wahame kijiji hapo lakini bibi yao aliondoka na kurejea baadaye.
Amesema watoto walikwenda matembezi kwa ruhusa ya mzazi na kuwa majina ya watuhumiwa yatatajwa.
Baba wa watoto hao, Respikius John amesema waliaga wanakwenda kucheza na wenzao.
Amesema baada ya kucheza walirejea nyumbani jioni na kubadili nguo na kuondoka tena lakini hawakuonekana hadi miili yao ilipokutwa kichakani.