Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Tido Mhando aachiwa huru

38361 Tidopic Tido Mhando aachiwa huru

Tue, 29 Jan 2019 Chanzo: mwananchi.co.tz

Dar es Salaam. Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu imemwachia huru aliyekuwa Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC), Tido Mhando.

Tido ameachiwa huru leo Ijumaa Januari 25, 2019 baada ya mahakama hiyo kumkuta hana hatia.

Hukumu hiyo imetolewa leo na  Hakimu Mkazi Mkuu, Huruma Shaidi baada ya upande wa mashtaka kushindwa kudhibitisha mashtaka yake.

Tido alifikishwa Kisutu kwa mara ya kwanza Januari 26, 2018, kujibu mashtaka matano.

Katika kesi hiyo ya uhujumu uchumi namba 7/2018, Tido alikabiliwa na mashtaka matano, mashtaka manne ni ya kutumia madaraka vibaya na moja la kuisababishia Serikali hasara ya Sh887.1 milioni.

Agosti 27, 2018 Mahakama hiyo ilimkuta Tido na kesi ya kujibu baada ya Hakimu Shaidi kupitia ushahidi uliotolewa na mashahidi watano wa upande wa mashtaka.

Baada ya Tido kukutwa na kesi ya kujibu, alianza kujitetea.

Katika utetezi wake, Tido alidai kuwa mchakato mzima wa kuingia ubia wa kuhamisha TBC kutoka katika mfumo wa analojia kwenda digitali ulifanywa na bodi ya TBC.

Akihojiwa na wakili wa Takukuru alidai kuwa hakuna kitu alichokifanya bila ridhaa ya bodi na bodi ndiyo iliyomuagiza afanye mchakato wa awali na ulipokamilika aliwasilisha kwao, mwaka 2009.

Alidai kwamba hadi anaondoka TBC hakuna mtu yeyote aliyezungumzia suala hilo, si Serikali wala bodi.

Tido alipoulizwa na wakili wa Takukuru juu ya tofauti za mkataba aliongia na kampuni ya Chanel 2 group na ule wa Startimes alidai aliandikishiana nao mkataba wa makubaliano ya awali kwa sababu walikuwa wakitaka kuhakikishiwa kama wangeitwa na bodi ya TBC na kwamba aliusaini yeye peke yake.

Aliongeza kuwa katika mkataba halisi walioingia na kampuni ya Startimes aliusaini yeye na mwanasheria wa TBC.

Alibainisha kuwa Mkataba wa Startimes ndiyo mkataba halisi ambao waliandikishiana baada ya bodi kuridhia.

Tido amedai kuwa kutokana na sheria na taratibu za manunuzi, mkataba halali wa TBC lazima usainiwe na watu wawili ambao ni Mkurugenzi na Mwanasheria na pia lazima uwe na muhuri wa shirika.

Oktoba 30, 2018, Tido kupitia mawakili wake Martin Matunda (marehemu kwa sasa) na Dk Ramadhani Maleta walifunga ushahidi wa upande wa utetezi.

Miongoni mwa mashahidi wa upande wa mashtaka waliotoa ushahidi katika kesi hiyo ni pamoja na ofisa uchunguzi wa Takukuru, Victor Lesuya, Mwanasheria wa TBC, Gwakisa Mlawa na Mkurugenzi Mkuu mstaafu wa TBC, Clement Mshana.

·Tido amtaja Kikwete mahakamani

Katika kesi hiyo inadaiwa kuwa Juni 16, 2008,   akiwa Dubai, Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE), Tido ambaye alikuwa mkurugenzi wa TBC, kwa makusudi alitumia madaraka yake vibaya kwa kusaini mkataba wa kuendesha na utangazaji wa vipindi vya televisheni kati ya TBC na Channel 2 Group Corporation (BV1) bila ya kupitisha zabuni, kitu ambacho ni kinyume na Sheria ya Manunuzi na kuinufaisha BVl.

Katika shtaka la pili, Tido anadaiwa kutumia vibaya madaraka yake Juni 20, 2008 aliposaini makubaliano kwa utangazaji wa digitali duniani kati ya TBC na BVl.

Katika shtaka la tatu, anadaiwa Agosti 11, 2008 na Septemba 2008 akiwa Dubai, Tido alitumia vibaya madaraka yake kusaini mkataba wa makubaliano kwa ununuzi, usambazaji kufunga vifaa vya usambazaji na mnara wa utangazaji kati ya TBC na BVI na kuifaidisha BVI.

Katika shtaka la nne, anadaiwa kuwa  Novemba 16, 2008 akiwa Dubai, Tido alitumia vibaya madaraka yake kusaini mkataba wa makubaliano kwa kuendesha miundombinu ya utangazaji (DTT Broadcast Infrastructure) kati ya TBC na BVI na kuinufaisha BVI.

Katika shtaka la mwisho,  anadaiwa kuwa kati ya Juni 16 na Novemba 16, 2008 akiwa UAE, Tido aliisababishia TBC hasara ya Sh887.1 milioni.

VIDEO: Hukumu ya Tido Mhando sasa Januari 25

 

·Wakili Takukuru akwamisha kesi ya Tido Mhando

 

·Tido: Tuhuma hizi zimeniumiza sana

 



Chanzo: mwananchi.co.tz