Tabora. Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa nchini Tanzania (Takukuru) inamshikilia Kaimu meneja wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) Wilaya ya Igunga, mkoani Tabora, John Mgeni kwa tuhuma za kuomba na kupokea rushwa.
Kaimu Mkuu wa Takukuru mkoa wa Tabora, Mussa Chaulo akizungumza na waandishi wa habari jana Alhamisi Novemba 14, 2019 alisema mtumishi huyo wa umma anadaiwa kuomba na kupokea rushwa kutoka kwa mmoja wa wafanyabiashara mjini Igunga kama kishawishi cha kutomchukulia hatua kwa makosa ya kutotoa stakabadhi za kielektroniki.
“Uchunguzi wa awali umebaini kuwa Kaimu meneja huyo ameomba na kupokea rushwa ya Sh2 milioni kutoka kwa mfanyabiashara huyo ambaye jina linahifadhiwa kwa sasa,” alisema Chaulo
Alisema mtuhumiwa atafikishwa mahakamani muda wowote uchunguzi wa awali utakapokamilika huku akionya kuwa yeyote atakayejihusisha na vitendo vya rushwa atakutana na mkono wa dola.