Dar es Salaam. Mkuu wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) Mkoa wa Kinondoni, Theresia Mnjagira amesema miradi 16 ya maendeleo ya Sh40 bilioni walioifanyia ukaguzi, nane imebainika kuwa na viasharia vya rushwa.
Mnjagira ametoa kauli hiyo leo Ijumaa Julai 12, 2019 wakati akitoa taarifa ya utendaji kazi wa miezi mitatu kuanzia Aprili hadi Juni, 2019 na kwamba miradi hiyo inatekelezwa Wilaya ya Ubungo na Kinondoni.
Ameitaja miradi yenye viashiria vya rushwa ina thamani ya zaidi ya Sh30 bilioni, ikiwemo ya ujenzi wa shule ya sekondari ya Kimara, ujenzi wa maktaba, jengo la utawala na maabara na ukarabati wa madarasa manne na ofisi ya walimu ya shule ya msingi Kulangwa.
"Kwanza taratibu za manunuzi kutofuatwa, fedha kutotolewa kwa utaratibu. Tumeshaanza uchunguzi ili kubaini ukiukwaji wa taratibu hizi na ikithibitika hatua stahiki zitachukuliwa," amesema Mnjagira.
Mnjagira amesema mojawapo ya majukumu ya Takukuru ni kufuatilia matumizi ya fedha za umma kuhakikisha miradi inatekelezwa kwa kiwango kinachotakiwa na thamani ya fedha iliyokusudiwa inapatikana.