Songea. Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa mkoani Ruvuma (Takukuru) inamshikilia Mhandisi wa maji wa Halmashauri ya Wilaya ya Nyasa, Evaristo Ngole kwa madai ya kushawishi na kupokea rushwa ya Sh9 Milioni kutoka kwa mkandarasi.
Akizungumza na Mwananchi ofisini kwake leo Jumatatu Juni 24, 2019, Kamanda wa Takukuru mkoani Ruvuma, Yustina Chagaka amedai kuwa mhandisi huyo aliomba fedha hizo kutoka kwa mkandarasi ili aweze kumpitishia malipo yake ya kazi ambazo alikuwa amezifanya wilayani humo.
Amesema mkandarasi huyo alitekeleza mradi wa maji katika vijiji vya Lilondo, Asili na Lumecha na kukamilika kwa wakati kutokana na mkataba wake wa kazi, alidai wakati akisubiri kulipwa, ndipo mhandisi huyo alipofikia hatua ya kumshawishi kwa kumwomba kiasi hicho cha fedha na kumtaka akaziingize kwenye akaunti yake iliyopo benki ya CRDB.
Kamanda huyo amesema mlalamikaji ambaye ndiye mkandarasi wa mradi huo unaotekelezwa katika vijiji hivyo wilayani, Nyasa, alidai aliingiza fedha hizo kwenye akaunti hiyo kwa awamu tatu.
Na awamu ya tatu aliwekewa mtego na kufanikiwa kukamatwa baada ya fedha hiyo kuingia kwenye akaunti yake.
Kamanda Yustina, amesema tatizo la rushwa linakwamisha miradi mingi ya maji mkoani Ruvuma.
Pia Soma
- RC Mwanri amsimamisha meneja wa TRA, aagiza uchunguzi uanze
- Wanawake wawili kizimbani Kisuti kwa kosa la utakatishaji fedha
- Wawili kizimbani kwa dawa za kulevya
Amesema Takukuru inatoa pongezi kwa makandarasi wote wanaozingatia weledi katika kutekeleza miradi ya maendeleo ili thamani ya fedha iweze kuonekana katika miradi hiyo na kuleta tija kwa Taifa.
Pia wanaendelea kuwaomba wananchi kuendelea kuunga mkono juhudi za mapambano dhidi ya rushwa kwa kukataa kujihusisha na vitendo vya rushwa na kutoa taarifa za vitendo hivyo katika ofisi za Takukuru kusudi wahusika wachukuliwe hatua za kisheria.