Tabora. Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) mkoani Tabora imeokoa Sh9.6 milioni katika kipindi cha miezi mitatu kuanzia Januari hadi Machi mwaka huu.
Kaimu mkuu wa Takukuru mkoa wa Tabora, Mashauri Elisante amesema fedha zilizookolewa zimerejeshwa kwenye akaunti ya mkurugenzi mkuu Takukuru iliyopo Benki Kuu.
Amesema fedha zilizookolewa ni zilizotokana na malipo hewa ya watumishi wa afya, malipo ya viwanja vya ‘block V’ vilivyopo manispaa ya Tabora ambavyo wamiliki wake hawakuvilipia wakati wanamilikishwa, ubadhilifu na ukiukwaji wa taratibu za malipo uliobainika katika uchunguzi wao.
Alisema katika kipindi hicho, jumla ya malalamiko 13 yalipokelewa na kufunguliwa majalada, kati ya hayo sita yamekamilika na kesi nne zipo mahakamani zinaendelea kusikilizwa.
Baadhi ya wananchi wameipongeza Takukuru kwa kazi nzuri inayofanya na kuitaka iendelee kuongeza kasi ya kushughulikia malalamiko ya rushwa.
"Bado kuna harufu ya rushwa katika baadhi ya taasisi hasa hospitali ya Kitete na idara ya ardhi, " amesema Thomas Aidan mkazi wa Kanyenye.
Naye Mwanahamisi Shaban ambaye ni mkazi wa Mwinyi manispaa ya Tabora ameitaka idara ya ardhi manispaa ya Tabora izidi kumulikwa kwa vile bado ina harufu ya rushwa.