Kisarawe. Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) wilayani Kisarawe, mkoani Pwani imempandisha kizimbani aliyekuwa ofisa tawala wilaya hiyo, John Mwendamaka akituhumiwa kushawishi na kupokea rushwa ya Sh2 milioni kinyume na kifungu cha 15(1) cha sheria ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa Na.11 ya 2007.
Mwendamaka amepandishwa mahakamani leo Jumatano Februari 20, 2019 katika mahakama ya wilaya ya Kisarawe.
Mwanasheria wa Takukuru wilayani humo, Naftali Mnzava ameiambia Mahakama kuwa Mwendamaka alitenda kosa hilo kati ya Aprili 1 hadi Aprili 30, 2016 ambapo akiwa ofisa tawala wa wilaya alishawishi apewe fedha hizo ili amwezeshe ndugu wa mtoa fedha kujiunga na Jeshi la Kujenga Taifa (JKT).
Mwanasheria huyo pia alitaja kosa la pili alilolifanya katika kipindi hicho wilayani humo ambapo alidai Mwendamaka alipokea fedha hizo kutoka kwa mtoaji, ili amsaidie ndugu yake kujiunga na JKT kinyume cha sheria.
Hata hivyo, Mwendamaka amekanusha mashitaka hayo na aliachiliwa kwa dhamana. Kesi hiyo imeahirishwa hadi Machi 5, 2019.