Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Sita kizimbani kwa kukutwa na meno ya tembo, kiboko

Wed, 18 Sep 2019 Chanzo: mwananchi.co.tz

Dar es Salaam. Watu sita wamefikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu wakikabiliwa na mashtaka manne, likiwemo la kukutwa na vipande 413 vya meno ya tembo na viwili vya meno ya kiboko, yote yakiwa na thamani ya Sh4.03 bilioni.

Washtakiwa hao ni Hassani Likwena (39), Bushiri Likwena, Oliver Mchuwa (35), Salama Mshamu (21), Haidary Sharifu (44) na Joyce Thomas (33).

Akizungumza leo Jumanne Septemba 17, 2019 mbele ya Hakimu Mkazi, Vick Mwaikambo wakili wa Serikali mwandamizi, Wankyo Simon amesema washtakiwa hao wanakabiliwa na mashtaka ya kushiriki genge la uhalifu, kukutwa na vipande vya meno ya tembo na kiboko pamoja na kutakatisha fedha.

Simon amedai kati ya Januari Mosi, 2017 na Septemba 3, 2019 maeneo tofauti Mkoa wa Mtwara , Pwani na Dar es Salaam washtakiwa walishiriki genge la uhalifu kwa kupokea nyara za Serikali;  vipande 413 vya meno ya tembo vyenye thamani ya Dola 1,755,000 za Marekani na vipande viwili vya meno ya kiboko vyenye thamani ya Dola 1500 za Marekani.

Katika shtaka la pili, Septemba 3, 2019 maeneo ya Saku Chamanzi  jijini Dar es Salaam, kwa pamoja walikutwa na nyara za Serikali ambazo ni meno hayo ya tembo bila ya kuwa na kibali cha mkurugenzi wa wanyamapori.

Simon amedai shtaka la tatu Septemba 3, 2019 maeneo ya Saku Chamanzi walikutwa vipande viwili vya meno ya kiboko kinyume na sheria mali ya Serikali bila ya kuwa na kibali cha mkurugenzi wa wanyamapori.

Pia Soma

Advertisement
Katika shtaka la nne inadaiwa tarehe tofauti kati ya Januari Mosi, 2017 na Septemba 9, 2019 washtakiwa kwa pamoja walikutwa na vipande 413 vya meno ya tembo na mawili ya kiboko wakati wakijua upokeaji huo ni viashiria vya kosa tangulizi ambalo ni ujangili.

Baada ya maelezo hayo wakili Simon amedai upelelezi wa shauri hilo bado haujakamilika, kuomba tarehe kwa ajili ya kutajwa.

Hakimu Mwaikambo amesema mahakama hiyo haina mamlaka ya kusikiliza shauri hilo, kuahirisha kesi hadi Oktoba Mosi, 2019.

Chanzo: mwananchi.co.tz