Dar es Salaam. Inspekta Jenerali wa Polisi (IGP), Simon Siro leo atazungumza na vyombo mbalimbali vya habari katika ukumbi wa makao makuu ya Jeshi la Polisi jijini Dar es Salaam.
Miongoni mwa mambo yanayotarajiwa kuzungumzwa na IGP Siro katika mkutano huo utakaoanza saa 4:00 asubuhi ni sakata la kutekwa kwa mfanyabiashara Mohammed Dewji ‘Mo Dewji ambalo limevuta hisia za watu wengi ndani na nje ya nchi.
Oktoba 13 Siro alilieleza Mwananchi kuwa polisi bado wanaendelea na upelelezi wa tukio la kutekwa kwa mfanyabiashara huyo.
Bilionea huyo alitekwa na watu wasiojulikana Alhamisi asubuhi ya Oktoba 11 katika hoteli ya Colosseum jijini Dar es Salaam alikokwenda kwa ajili ya kufanya mazoezi.