Arusha. Shehena ya madini ya vito aina mbalimbali ikiwepo madini ya Tanzanite imekamatwa ikiwa inasafirishwa kinyume na taratibu kwenda nchi jirani ya Kenya.
Madini hayo zaidi ya kilo 36 yamekamatwa jana Jumatano Juni 26, 2019 na askari maalum ya intelijensia baada ya kupata taarifa madini hayo kutoroshwa kutoka Arusha katika basi la Perfect trans ambalo hufanya safari kutoka Arusha hadi Nairobi nchini Kenya.
Mkuu wa wilaya ya Longido, Frank Mwaisumbe amesema madini hayo ikiwepo Tanzanite kilo tano, Ruby na Greentonaline yalikuwa yanasafirishwa kwenye mfuko mkubwa yakiwa yamechanganywa na mchele.
"Tulipata taarifa za kusafirishwa madini haya na askari wakitumia mbwa waliweza kuyabaini katika gari," amesema
Amesema dereva wa gari hilo na kondakta wake wanashikiliwa kwa mahojiano wakidai hawamjui mmiliki wa madini hayo.
"Wanasema madini walikabidhiwa na mwendesha bodaboda Arusha na kuwa wangefika Namanga (mpakani mwa Tanzania na Kenya) kuna mtu ambaye walipewa namba ya simu angefika kuchukua," amesema.
Pia Soma
- Zitto ataka Bunge kuibana Serikali ya Tanzania kuhusu kukopa
- Tiba asili za barabarani zapigwa marufuku Iringa
- Nyama ya nyumbu yampandisha kortini mtumishi wa hifadhi ya Ikona
- Kiongozi wa mbio za Mwenge amgomea Mkuu wa Wilaya ya Mwanga
Ofisa madini mkazi wa mkoa Arusha, Erick Robert anatarajia kutoa thamani ya madini hayo na aina zake pindi wakikamilisha kuyapima.