Dar es Salaam. Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu imeshindwa kusikiliza ushahidi katika kesi inayomkabili aliyekuwa Mkurugenzi mtendaji wa Shirika la Maendeleo ya Petrol Tanzania (TPDC), James Mataragio na wenzake baada ya upande wa mashtaka kutokuwa na shahidi.
Wakili wa Serikali, Fatuma Waziri alidai mbele ya Hakimu Mkazi Mfawidhi Kelvin Mhina kuwa shauri hilo lilikuja kwa ajili ya usikilizwaji lakini shahidi aliyetarajiwa kutoa ushahidi anaumwa, hivyo aliiomba Mahakama iahirishe shauri hilo.
Baada ya maelezo hayo, Hakimu Mhina alikubaliana na ombi hilo na kuahirisha shauri hilo hadi Juni 20,2019 kwa ajili ya usikilizwaji.
Mbali na Mataragio, washitakiwa wengine ni George Semi, Mkuu wa Kitengo cha Fedha, Wellington Hudson, Mkurugenzi wa mipango na mkakati, Kelvin Komba ambaye pia alikuwa mkurugenzi na Edwin Riwa Meneja wa kitengo cha ununuzi.
Katika kesi hiyo, washitakiwa hao wanadaiwa kuwa kati ya Aprili 8,2015 na Juni 3, 2016, wakiwa watumishi wa umma na waajiriwa wa TPDC kwa nafasi zao, wakati wakitimiza majukumu yao kwa makusudi, walitumia madaraka vibaya.
Ilidaiwa walibadilisha na kupitisha bajeti na mpango wa mwaka wa manunuzi wa mwaka 2014/2015 na 2015/2016 kwa kuingiza ununuzi wa kifaa cha utafiti cha airborne gravity gradiometer survey ndani ya Ziwa Tanganyika bila kibali cha bodi ya wakurugenzi ya shirika.
Pia Soma
- Wizara ya Sheria na Katiba yasema ndoa kwa wahanga wa udhalilishaji husababisha kesi za udhalilishaji kutomalizika
- Kiongozi mbio za mwenge awaasa wahandisi
- Ramaphosa ateua mpinzani kuwa waziri