Dar es Salaam. Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu imeutaka upande wa mashtaka katika kesi ya kurekodi video ya ngono na kuisambaza katika mitandao ya kijamii inayomkabili mlimbwende wa Tanzania 2006, Wema Sepetu kuleta mashahidi wengi kadri inavyowezekana.
Hayo yameelezwa leo, Jumatatu, Machi 18,2019 na Hakimu Mkazi, Maira Kasonde baada ya wakili wa Serikali Glori Mwenda kudai mahakamani hapo kuwa shahidi aliyekuwa ameandaliwa yuko safarini Arusha kikazi.
“Kesi hii imekuja kwa ajili ya kuanza kusikilizwa na leo tulitakiwa kuwa na shahidi, lakini yuko safarini Arusha kikazi, hivyo tunaomba tarehe nyingine kwa ajili kuendelea,” amedai wakili huyo.
Wakili wa utetezi, Ruben Semwanza amedai hawana pingamizi kama shahidi hayupo, lakini wanapaswa kuwa na mawasiliano na shahidi kama hayupo waje nao wengine.
Baada ya maelezo hayo, Hakimu Kasonde ameutaka upande wa mashtaka kuleta mashahidi wengi kadri inavyowezekana na kuahirisha kesi hiyo Aprili 18, 2019 itakapoendelea.
Katika kesi hiyo, Wema anadaiwa Oktoba 15, 2018 katika maeneo mbalimbali jijini Dar es Salaam alirekodi video ya ngono na kuisambaza katika mtandao wake wa Instagram.