Kesi ya uhujumu uchumi inayomkabili aliyekuwa Mkuu wa Wilaya ya Hai, Lengai Ole Sabaya na wenzake sita imeahirishwa baada ya shahidi wa Jamhuri kudai bado anaumwa.
Afisa wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru), Ramadhan Juma alitegemea kutoa ushahidi wake leo Ijumaa Oktoba 22, 2021, lakini Wakili Mwandamizi wa Serikali, Felix Kwetukia aliiomba Mahakama ya Hakimu Mkazi Arusha iahirishe kesi hadi Oktoba 27, 2021 kwa kuwa shahidi huyo afya yake bado haijaimarika.
Mawakili wa utetezi walipinga ombi hilo na kuiomba mahakama iamuru Jamhuri iwalete mashahidi wengine ili shauri hilo liendelee kusikilizwa.
“Mahakama imeona uthibitisho wa kuugua kwa shahidi wa saba umeletwa na muda wa kutoa hati ya wito kwa mashahidi wengine umekuwa mfupi, hivyo mahakama imeona busara kuahirisha kesi hiyo hadi Oktoba 27, 2021” alisema Hakimu Mkazi, Patricia Kisinda.