Dar es Salaam. Ofisi ya Wakala wa Maabara ya Mkemia Mkuu wa Serikali imepokea sampuli za mabaki yanayodaiwa kuwa ya Naomi Marijani, anayedaiwa kuuawa na mumewena mwili wake kuteketezwa kwa moto.
Ofisi hiyo imesema itafanyia kazi sampuli hizo ndani ya muda mfupi.
Inadaiwa kuwa mume huyo, Khamisi Luwongo ambaye yupo mikononi mwa Polisi alimuua mkewe na baadaye kutumia magunia mawili ya mkaa kuchoma maiti yake na kisha kufukia majivu yake katika shamba lake lililoko Kijiji cha Marogoro kilichopo wilayani Mkuranga.
Kwa mujibu wa polisi, baadaye mume huyo alienda kituo cha polisi kutangaza kuwa mkewe, ambaye ni mama wa mtoto mmoja, ametoweka nyumbani kwake Gezaulole-Kigamboni tangu Mei 15.
Akizungumza na Mwananchi jana, Mkemia Mkuu wa Serikali, Dk Fidelice Mafumiko alisema sampuli hiyo iliwasilishwa jana katika maabara kwa ajili ya kipimo cha vinasaba (DNA) na kazi ya uchunguzi inaanza leo.
Dk Mafumiko alisema uchunguzi wa aina hiyo huchukua hadi siku 21, lakini kutokana na uharaka wa suala hilo itafanyika ndani ya muda mfupi na kwa kuzingatia weledi.
Habari zinazohusiana na hii
- VIDEO: Majirani wamlilia mwanamke anayedaiwa kuuawa na mumewe
- VIDEO: Eneo linalodaiwa kufukiwa mabaki ya mwili wa Naomi Marijani
Kaka wa Naomi, Wiseman Marijani alisema ofisi hiyo imewaahidi kulishughulikia suala hilo kwa haraka na majibu yatakapopatikana wataweka msiba.
“Kama tuliweza kuvumilia kwa zaidi ya siku 60 tukiwa hatufahamu lolote kuhusu ndugu yetu alipo, hatuwezi kushindwa (kusubiri) sasa, alisema Wiseman.