Kesi ya uhujumu uchumi inayomkabili aliyekuwa Mkuu wa Wilaya ya Hai, Lengai Ole Sabaya na wenzake sita leo Jumatano Machi 16, 2022 imeahirishwa kwa muda baada ya mshtakiwa huyo wa kwanza (Sabaya) kusema anajisikia vibaya na kuomba kupumzika.
Shauri hilo limeahirishwa saa 7:03 mchana na Hakimu Mkazi Patricia Kisinda anayesikiliza shauri hilo baada ya mshitakiwa huyo kusimama, kuvua barakoa na kuieleza mahakama kuwa hajisikii vizuri anaomba apumzike ila shauri hilo liendelee kwa kuwa mawakili wake wapo.
Awali Mawakili wa Jamhuri walipinga ombi hilo, ambapo baadaye waliridhia na kueleza mahakama kwa kuwa mshitakiwa huyo ameruhusu shauri liendelee bila uwepo wake.
Wakili Mosses Mahuna anayemtetea Sabaya aliieleza mahakama kuwa hakuna sababu ya msingi ya kuahirisha kesi hiyo kwani mshitakiwa ameruhusu kesi iendelee mbele ya mahakama na hii si mara ya kwanza shauri hilo kuendelea bila uwepo wa mshitakiwa huyo.
Wakili Mahuna aliieleza mahakama kuwa mteja wake Sabaya anaumwa tangu asubuhi ila alikuwa amejikaza.
Hayo yametokea wakati Wakili wa Serikali, Neema Mbwana, alisimama na kutaka kuanza kumuuliza maswali ya dodoso shahidi wa nane wa utetezi Nathan Msuya ambaye ni mshitakiwa wa saba katika kesi hiyo.