Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

"Sabaya alifanya ujambazi dukani" - Shahidi

44a01984fa73e97c86f8f43d471342ad Ole Sabaya

Wed, 4 Aug 2021 Chanzo: www.habarileo.co.tz

SHAHIDI wa sita katika kesi ya unyang’anyi wa kutumia silaha na uporaji wa mali na Sh milioni 3,159,000 inayomkabili aliyekuwa Mkuu wa Wilaya ya Hai, Lengai Ole Sabaya na wenzake wawili, amedai mahakamani kuwa Sabaya na wenzake walifanya ujambazi na hayakuwa maagizo ya Rais John Magufuli.

Sabaya, Silvester Nyengu (26) na Daniel Mbura (38) wanaokabiliwa na kesi hiyo, wanadaiwa kuvamia dukani na kupora mali na fedha Februari 9, mwaka huu.

Shahidi huyo, Bakari Msangi alidai katika Mahakama ya Hakimu Mkadhi Mkoa wa Arusha jana kuwa, Sabaya na wenzake walitumia silaha kupora katika duka la Shahiid Store katika mtaa wa Bondeni jijini Arusha na haamini kama yalikuwa maagizo ya Magufuli.

Msangi alidai hayo wakati akihojiwa na Mwanasheria Mwandamizi wa Serikali, Abdallah Chavula mbele ya Hakimu Mwandamisi wa Serikali, Odira Amworo baada ya kumaliza kuhojiwa na mawakili wa utetezi.

Msangi alidai kama kweli Sabaya aliagizwa na Rais Magufuli angemjulisha Mkuu wa Wilaya ya Arusha kuhusu jambo hilo.

Chavula alipomuuliza ni kwa nini maelezo ya polisi aliyoandika February 10, mwaka huu yanatofautiana na maelezo aliyoyatoa mahakamani, Msangi alidai ni kwa sababu mpelelezi wa kesi askari kanzu aliyemtaja kwa jina la Callebu aligoma kumsomea mara alipomaliza kuandika.

Msangi alidai kuwa askari huyo alikuwa akimshawishi kumaliza kesi hiyo nje ya Mahakama kwa madai alitumwa na Sabaya na viongozi wengi wa serikali ngazi ya juu.

Chavula pia alimtaka shahidi huyo aieleze Mahakama sababu za Sabaya kuondolewa katika nafasi ya uenyekiti wa Umoja wa Vijana Mkoa wa Arusha (UVCCM).

Msangi alidai uamuzi huo ulifanywa baada ya Sabaya kujifanya ofisa wa usalama wa taifa na kuchongesha kitambulisho na kufikia hatua serikali kumshitaki.

Alidai Katibu wa jumuiya hiyo taifa wakati huo, Shaka Hamdu Shaka aliitisha kikao cha Baraza Kuu Taifa na kumsimamisha na hakurudishwa tena kwenye nafasi hiyo.

Msangi alidai vitendo alivyofanya Sabaya na wenzake dukani kwa Mohamed Al Saad ni ujambazi, unyang’anyi, uporaji, utekaji na kumtishia kumuua na hawakuwa watumishi wa Mamlaka ya Mapato (TRA) wala Polisi.

Alidai msaidizi wa Sabaya ambaye ni mshitakiwa wa pili, Silverster Nyengu hakumpiga, hakumpekua na hajawahi kumtishia kwa risasi na muda wote alikuwa amekaa naye kwenye gari alikuwa kimya na yeye alidhani mshitakiwa huyo ni bubu.

Chavula alimuuliza kama pale dukani kwa Mohamed Al Saad ulivamia au ulifanya kitu gani, Msangi alisema hakuvamia kwani alipigiwa simu na Ally Al Saad Hajirini kama rafiki na ndugu kwenda kutoa msaada.

Chanzo: www.habarileo.co.tz