Tabora. Jeshi la Polisi mkoani Tabora linawashikilia watu saba kwa tuhuma za kukutwa na magunia 57 ya dawa za kulevya aina ya bangi pamoja na magunia mawili ya mbegu za zao hilo.
Akizungumza leo Jumatatu Septemba 24, 2018 Kamanda wa Polisi mkoani hapa, Emmanuel Nley amesema watu hao wamekamatwa usiku wa kuamkia leo katika kitongoji cha Kanolo kata ya Igulungu wilaya ya Uyui.
Amesema polisi walipewa taarifa na wakati wakiwa kwenye doria walifanikiwa kuwakamata watu hao wakiwa na kiasi hicho kikubwa cha bangi.
Amesema watuhumiwa hao walikutwa na pikipiki mbili walizokuwa wakizitumia kusafirisha bangi.
Amebainisha kwamba bangi hiyo ilikuwa isafirishwe kwenda maeneo mbalimbali nchini ikiwemo Mwanza, Tarime mkoani Mara na Dar es salaam.
Kamanda Nley amesema watuhumiwa watafikishwa mahakamani upelelezi ukikamilika.