Moshi. Mahakama ya Hakimu Mkazi Moshi imewatoza faini ya Sh100 milioni, raia wawili wa Thailand, walioingia nchini na kiasi kikubwa cha fedha bila kuzitolea taarifa kwa idara ya ushuru ya Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA).
Raia hao wa Thailand, Pukjira Thanda (56) na Anuwat Charcentam (58) waliingia nchini na Dola 174,320 za Marekani, sawa na zaidi ya Sh400 milioni za Tanzania kupitia uwanja wa ndege wa Kimataifa wa Kilimanjaro (KIA) Julai 10, mwaka huu.
Wafanyabiashara hao walifikishwa mahakamani jana Julai 13, 2018 mbele ya Hakimu Mkazi, Sophia Masati na kusomewa mashtaka yao na wakili mwandamizi wa Serikali, Omary Kibwana aliyesaidiana na wakili wa Serikali, Kassim Nassir.
Washitakiwa hao walikiri kosa hilo na ndipo Hakimu Masati alipowatoza faini ya Sh100 milioni kwa kushindwa kuzitolea taarifa (declare), fedha hizo kama sheria inavyotaka fedha zinazozidi Dola 10,000 zitolewe taarifa kwa maofisa wa TRA.