Dar es Salaam. Mfanyabiashara raia wa Kenya, Raphael Ongangi anayedaiwa kutekwa na watu wasiojulikana maeneo ya Oysterbay, Dar es Salaam nchini Tanzania amepatikana akiwa hai leo Jumanne Julai 2, 2019 Mombasa, Kenya.
Raphael anadaiwa kutekwa na watu hao Juni 24, 2019 akiwa na mke wake Veronica Kundya walizuiwa kwa mbele na kuwatolea silaha aina ya bastola na kuwachukua wote wawili kabla ya kumwachia mkewe na kuondoka na Raphael.
Akizungumza na Mwananchi, Veronica amethibitisha kupatikana kwa mumewe huyo asubuhi ya leo Jumanne.
Amesema mumewe amepatikana Mombasa nchini Kenya, “Nimezungumza naye mwenyewe yupo Mombasa, tumezungumza kwa kifupi nashukuru sana, mmenisaidia (Mwananchi),” amesema Kundya akiwa na furaha
Mchana wa leo Jumanne, Veronica ameandika ujumbe unaozungumzia kupatikana kwa mme wake. Ujumbe huo ulisomeka
“Nina haraka sana sitaweza kusema mengi zaidi ya kumshukuru Mungu sana sana kwa kuwa yeye ni Mungu wa miujiza na kuwashukuru wote kwa moyo wangu wote kwa sala na kujitoa kwenu kwenye kipindi hiki kigumu cha mimi na familia yangu.”
Habari zinazohusiana na hii
- Zitto azungumzia akaunti zake kudukuliwa, Nape na Bashe nao walonga
- Zitto awasha moto bungeni Tanzania
- Kutekwa kwa raia wa Kenya, Zitto aiomba Serikali ya Tanzania
Raphael amepatikana ikiwa ni siku moja tangu Kiongozi wa chama cha upinzani Tanzania cha ACT-Wazalendo, Zitto Kabwe kuzungumza na waandishi wa habari kuhusu tukio hilo lililomkuta rafiki yake wa karibu ambaye miaka ya nyuma alikuwa msaidizi wake.