JESHI la Polisi mkoani Rukwa linawashikilia watu 24 kwa makosa ya utapeli wa mitandaoni ikiwemo kutumia Vitambulisho vya Taifa (NIDA ) vya watu wengine kutengeneza laini za simu za kitapeli.
Kamanda wa polisi mkoa wa Rukwa, William Mwanampaghale alithibitisha kuwa watuhumiwa hao maarufu, “wazee wa tuma kwenye namba hii” wengi wao vijana wamekatwa juzi kufuatia msako uliofanyika katika maeneo mbalimbali katika mji wa Sumbawanga, mkoani humo.
Alisema kuwa watuhumiwa walikamatwa na simu janja za kupakua 'programu tumishi' (apps) zenye uwezo wa kutuma ujumbe mfupi wa maneno kati ya 4,000 hadi 6,000 kwa wakati mmoja.
Alibainisha kuwa wakati wanakamatwa walikuwa wanaendelea kuzituma ujumbe wa kitapeli zenye ujumbe "tuma kwenye namba hii" kwa wananchi.
Pia watuhumiwa hao wamekamatwa na vipeperushi vyenye namba za simu za waganga wa kienyeji feki ambavyo wanavibandika mitaani ili wapita njia wasome namba hizo.
“Isitoshe tumewakamata wakiwa na tunguli, wanasesere wamevalishwa shanga na misumari na dawa za miti shamba ili wateja wao waamini kuwa ni waganga wa kienyeji wenye uwezo wa kuwasafishia nyota" alieleza.
Aidha aliwatahadharisha wakazi mkoani humo kujiepusha na matapeli hao kwamba wasikae kimya watoe taarifa katika mamlaka husika ili hatua kali zichukuliwe dhidi yao.