Jeshi la Polisi mkoani Arusha limesema kijana Patrick Mmasi (19) anayetuhumiwa kumuua mama yake, Ruth Mmasi ametoa ushirikiano uliosaidia kupatikana kwa vielelezo vya tukio hilo.
Mwili wa Mmasi aliyekuwa mfanyabiashara wa Madini ulikutwa kwenye chemba ya choo katika nyumba aliyokuwa akiishi na mwanaye huyo eneo la Njiro, jijini Arusha, Desemba 24 mwaka huu, baada ya kutoonekana tangu Desemba 11, 2021.
Kamanda wa Polisi Mkoa Arusha, Justine Masejo ameviambia vyombo vya habari leo Jumanne Desemba 28, 20201 Jeshi la Polisi linaendelea na uchunguzi wa tukio hilo.
"Bado tunamshikilia mtu mmoja kwa mahojiano ya kina juu ya tukio hilo ambalo lilipelekea umauti wa marehemu Ruth Mmasi,"amesema
Amesema chanzo cha tukio hilo bado kinachunguzwa na akawaomba wananchi, ndugu na jamaa kuwa wavumilivu wakati polisi wakiendelea na uchunguzi.
Mfanyabiashara huyo alizikwa jana katika Kijiji cha Migungani, Wilaya Arumeru, mkoani Arusha. Ameacha mtoto Mmoja Patricia ambaye anasoma nchini China.