Jeshi la polisi nchini limetangaza kuunda kikosi maalum kitakachofanya uchunguzi wa tukio la kuuawa kwa watu sita wa familia moja katika kijiji cha Kiganza halmashauri ya wilaya Kigoma mkoani kigoma usiku wa kuamkia Jumapili.
Kamishna wa operesheni na mafunzo wa jeshi la polisi nchini,kamishna wa Polisi Liberatus Sabas alisema hayo akizungumza na waandishi wa habari eneo la tukio ikiwa ni utekelezaji wa maagizo ya Mkuu wa jeshi la polisi nchini (IGP)Simon Sirro.
Sabas alisema kuwa hakuna atakayepona ambaye amehusika na tukio hilo na kwamba polisi wakisaidiana na vikosi vingine vya ulinzi na usalama wameanza kazi kuhakikisha wahalifu wote waliohusika na tukio hilo wanakamatwa haraka iwezekanavyo.
Kamishna huyo wa Operesheji na mafunzo wa jeshi la polisi alisema kuwa tayari timu ya wataalam wa uchunguzi imeshaanza na timu nyingine ya uchunguzi ya jeshi la polisi kutoka makao makuu ya polisi Dododma ipo njiani kwa ajili ya kuja kushiriki kwenye zoezi la uchunguzi na upelelezi kuwatafuta wahalifu waliohusika na tukio hilo. “Hakuna mtu yeyote aliyehusika anayeweza kukwepa mkono wa dola hivyo tumejipanga kuhakikisha watu hao wanakamatwa,tunaowamba wananchi wa eneo hilo kutoa taarifa ambazo zitalisaidia jeshi la katika kufaniki upelelezi wake,”Alisema Kamishna Sabas
Pamoja na yote Kamishana huyo wa operesheni na mafunzo amewaonya watu wenye taarifa kuhusiana na tukio hilo kutoa taarifa hizo sasa lakini wakaficha au kuwa ni sehemu ya tukio hilo wakibainika watashughulikiwa ipasavyo.
“Lazima jibu lipatikane ndani ya muda mfupi, kuna watu wameingiwa na pepo la kukosa hofu ya Mungu na kuwauwa wenzao kama kuku, Naomba wote wenye taarifa au kufahamu chochote kuhusiana na tukio hilo watoe taarifa na taarifa hizi zitakuwa za siri na watoa taarifa wote watalindwa ukiacha na tukajua itakuwa tatizo kubwa kwako,”alisema Mkuu huyo wa Operesheni na Mafunzo
Katika hatua nyingine mtoto James Januari (4) aliyelazwa Hospitali ya mkoa Kigoma Maweni baada ya kujeruhiwa vibaya kwenye tukio hilo anaendelea na matibabu hospitalini hapo.