Bagamoyo. Polisi wilaya ya Bagamoyo mkoani Pwani wamekamata madumu 30 ya lita 20 ya mafuta ya kula aina ya Mico Gold yanayodaiwa kuingizwa kimagendo kutoka nchini Malaysia.
Mafuta hayo yamekamatwa ikiwa ni siku 22 zimepita tangu mafuta mengine aina hiyo zaidi ya madumu 350 kukamatwa.
Kamanda wa polisi mkoani Pwani, Wankyo Nyigesa akizungumza leo amesema mafuta hayo yamekuwa yakiingizwa nchini kupitia bandari bubu wilayani humo na kwamba hayajalipiwa ushuru.
Amesema katika uchunguzi wao wa awali wamebaini mafuta hayo yamekutwa yakiwa hayana udhibitisho wa viwango kutoka Shirika la Viwango Tanzania (TBS) hali ambayo inatishia usalama wa afya za walaji.
Kamanda Nyigesa amesema katika tukio la jana madumu hayo 30 ya lita 20 yalikamatwa yakiwa yanasafirishwa kwa kutumia gari aina ya Nissan mali ya M. M. Seif wa Dar es Salaam, ambapo dereva wake alikimbia mara baada ya kuona askari.
"Uchunguzi wa awali umebaini mafuta haya yameingizwa kutoka nchi ya Malaysia na kupitishwa katika bandari bubu mojawapo huko Bagamoyo na kukwepa ushuru wa Serikali,” amesema
Kamanda huyo amesema kwa sasa madumu hayo pamoja na gari lililohusika kusafirisha yamehifadhiwa polisi Bagamoyo na kumtaka mmiliki wa Nissan hiyo kufika kituo chochote cha polisi kwa ajili ya kuhojiwa.
Mwisho