Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Polisi wakamata majahazi yakisafirisha mikoko

8982 Mikoko+pic TZW

Tue, 12 Jun 2018 Chanzo: mwananchi.co.tz

Dar es Salaam. Jeshi la Polisi kikosi cha wanamaji, limekamata watuhumiwa 16 na majahazi manne yakiwa na mali za magendo.

Akizungumza leo, Jumanne Juni 12 Kamanda wa polisi kikosi cha wana maji, Evance Mwijage amesema watuhumiwa hao wamekamatwa katika msako uliofanyika kwa kipindi cha wiki mbili.

Amesema katika kisiwa cha Sinda jumla ya watuhumiwa watano walikamatwa wakiwa na jahazi liitwalo ‘SV Mali SI HOJA’ likiwa limebeba miti ya mikoko likitokea Kibiti, Pwani.

"Katika msako tuliofanya kwa wiki mbili tumekamata wahalifu maeneo mbalimbali ndani ya bahari ikiwemo kisiwa cha Sinda wakiwa na jahazi lisilosajiliwa likiwa na mikoko ipatayo 500" amesema Mwijage.

Katika tukio jingine watu wanne wamekamatwa wakiwa na Jahazi lenye namba za usajili Z 1667 SV, likitokea Bagamoyo kwenda Zanzibar katika eneo la Pungume, likiwa limebeba miti ya mikoko 3,000 bila kibali.

 

Ameongeza katika tukio lingine watuhumiwa  saba wamekamatwa eneo la Pemba Mnazi, Kigamboni wakiwa na jahazi ambalo halina namba za usajili.

"Katika msako huo watuhumiwa wengine saba wakiwa na jahazi lililobeba mbao zinazokadiriwa kufikia 1,000 za miti aina ya mtondoo tuliwakamata eneo la Pemba Mnazi, Kigamboni wakitokea Msumbiji kwenda Zanzibar bila kibali, " ameongeza

Watuhumiwa wote wanaendelea kushikiliwa wakati upelelezi ukiendelea ili kuwabaini wamiliki wa majahazi hayo na baada ya kukamilika watafikishwa mahakamani.

Amesema kutokana na matukio ya uhalifu ikiwemo usafirishaji wa magendo, dawa za kulevya na uharamia, jeshi hilo litaendelea kufanya doria kuhakikisha sheria zinafuatwa.

 

Chanzo: mwananchi.co.tz