Kibaha. Polisi mkoani Pwani wamekamata televisheni saba na vifaa mbalimbali ikielezwa kuwa vimeibiwa maeneo mbalimbali wilayani Kibaha na Bagamoyo.
Vifaa hivyo vimepatikana baada ya polisi kufanya ukaguzi na kuwakamata watuhumiwa 35.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Pwani, Wankyo Nyigesa akizungumza leo Jumatano Aprili 15, 2020 amesema kati ya televisheni hizo, tatu zilitambuliwa na wamiliki.
"Wakati wote wa sikukuu sisi tulikua kazini, pamoja na mambo mengine tulifanya msako na kukamata watuhumiwa 35 wa makosa ya wizi, uvutaji bangi, unywaji pombe ya moshi maarufu gongo na kupatikana na silaha na tulipowahoji wote walikiri hivyo tunawapeleka mahakamani wakajibu tuhuma zao, "amesema Nyigesa na kutaja vifaa vingine kuwa ni spika na deki.
Amesema vifaa hivyo vimehifadhiwa polisi kusubiri taratibu nyingine zikamilike ili wamiliki wapatiwe.
Amesema watu wengine wanne wanashikiliwa na polisi baada ya kukutwa na bastola katika gari wakati wakiwa safarini kutoka Dar es Salaam kwenda Morogoro.