Mwanza. Polisi Mkoa wa Mwanza nchini Tanzania limewakamata watu 46 kwa makosa manne tofauti likiwemo la mauaji na wizi wa transfoma ya umeme mali ya Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco).
Ndani ya kipindi cha miezi miwili zaidi ya watu 96 wamekamatwa na polisi mkoani humo kwa tuhuma za vitendo vya uhalifu mbalimbali kutokana na operesheni zinazoendelea.
Akizungumza na waandishi wa habari leo Jumapili Septemba 22, 2019 Kamanda wa Polisi wa Mkoa huo, Jumanne Muliro amesema tukio la kwanza wanashikiliwa watu wanne kwa tuhuma za kumuua askari mgambo Nickson Mabuku.
Amesema tukio hilo lilitokea jana Jumamosi katika Kisiwa cha Bezi wilayani Ilemela ambapo walimshambulia mgambo huyo wakati akitekeleza majukumu yake wakipinga kitendo cha kukamatwa Laurent Joseph kwa tuhuma za wizi.
“Walimshambulia kwa silaha za jadi kisha kumzamisha ziwani na kusababisha kifo chake,” amesema kamanda Muliro
Katika tukio la pili, Kamanda Muliro amesema wamewakamata watu wawili wakiwa na transfoma mali ya Tanesco eneo la Mwaloni Kirumba ambayo iliibwa katika wilaya ya Sengerema.
Pia Soma
- Serikali ya Tanzania yahubiri umuhimu wa elimu
- Ras Jeshi asema wajasiriamali wanataka faida kubwa
- Phoenix Tanzania yatoa msaada kwa yatima Dar
- Waziri Kabudi aipongeza Airtel kwa kuzindua huduma za kifedha Afrika Mashariki
Kamanda huyo amesema katika msako ulioza Septemba 16 hadi 21, 2019 wamekamata watuhumiwa 12 wanaojihusisha na utengenezaji, uuzaji, unywaji wa pombe haramu ya moshi ambapo walikamata lita 110, mitambo mitano na mapipa sita ya pombe hiyo.
Kamanda Muliro amesema watuhumiwa 23 kati ya 46 wameshafikisha a mahakamani na kesi zao zinaendelea.