Iringa. Mkuu wa Wilaya (DC) ya Iringa Mjini nchini Tanzania, Richard Kasesela amesema polisi wilayani humo linamshikilia mkazi wa Semtema, Anord Mlay kwa tuhuma za kulawiti na kubaka watoto wadogo.
Akizungumza na Mwananchi leo Jumamosi Desemba 28, 2019, kwa simu, Kasesela amesema mtuhumiwa huyo alikamatwa wiki mbili zilizopita na alizuia dhamana kutokana na ukubwa wa matukio aliyofanya.
"Mtuhumiwa alikamatwa na nilizuia dhamana kwa sababu kuu mbili, kwanza iwapo angetoka wananchi wangemuua, pili simpendi kutokana na tukio hilo la ubakaji, hivyo mpaka sasa yupo rumande," amesema
Kuhusu taarifa kuwa amekwisha kuhukumiwa, Kasesela ambaye ni mwenyekiti wa kamati ya ulinzi na usalama ya wilaya hiyo amesema hana taarifa ya mtuhumiwa huyo kama ameshapelekwa mahakamani bali anachojua yupo rumande na wanangoja upelelezi kukamilika ndio apelekwe mahakamani.
"Ninachojua yupo mahabusu, sidhani kama kahukumiwa kwa sababu kwanza Mahakama ipo likizo na sina taarifa ya kesi yake kuanza kusikilizwa," amesema
Jitihada za kumpata kamanda wa polisi Mkoa wa Iringa zinaendelea ili aweze kuzungumzia tukio hilo.