Dar es Salaam. Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam nchini Tanzania linawashilia watu watatu waliojihusisha na maandamano katika ubalozi wa Afrika Kusini nchini Tanzania kushinikiza ndege ya Shirika la Ndege Tanzania (ATCL) iliyozuiwa nchini humo kuachiwa.
Takriban watu zaidi ya 100 waliandamana jana Jumatano katika ubalozi huo Posta jijini Dar es salaam huku wakiwa na mabango yenye ujumbe mbalimbali, wakisema kuzuiwa kwa ndege hiyo si jambo sahihi.
Kamanda wa kanda hiyo, Lazaro Mambosasa akizungumza na waandishi wa habari leo Alhamisi Agosti 29,2019 amesema kuna vijana walifanya maandamano hayo ili kuonyesha hisia zao kutoridhika kukamatwa kwa ndege yao.
Mambosasa amesema walipigiwa simu kuwa kuna watu wanaandamana kwenda ubalozi huo huku wakiwa na mabango mbalimbali ndipo alitoa maelekezo kwa maofisa wake wa jeshi la polisi akiwemo Kamanda wa Polisi mkoa Ilala ambao walifika eneo la tukio na walifanikiwa kuwatawanya waandamanaji hao.
“Kati ya waandamanaji hao watu watatu walikamatwa kwa bahati mbaya majina yao sijayachukua, watafikishwa kwenye vyombo vya sheria,” alisema Mambosasa.
Ndege hiyo ilizuiwa Agosti 23, 2019 katika uwanja wa Ndege wa Oliver Tambo kwa amri ya Mahakama ya Geuteng, Johnnesburg Afrika Kusini.
Habari zinazohusiana na hii
- Mamia waandamana Dar kushinikiza ndege ya Tanzania iliyozuiwa Afrika Kusini kuachiwa
- Polisi yawakamata wanaodaiwa kuratibu maandamano kudai ndege ya Tanzania kuachiwa
Wakati huo huo, Kamanda Mambosasa amesema wamewaua watu watatu wanaodhaniwa kuwa majambazi wakiwa na silaha mbalimbali ikiwemo shortgun katika maeneo ya Pugu, Dar es Salaam.
Mambosasa aliwataja waliouwawa ni Omary Athuman, Fullsaba na Babu Shobo na Dogo Side alifanikiwa kukimbia kusikojulikana hivyo jeshi la polisi linaendelea kumtafuta.