Habari

Burudani

Michezo

Biashara

Afrika

Live Radio

Nchi

Kijamii

Lifestyle

SIL

Polisi Dar wamsaka mume anayedaiwa kumuua mke

Muliroooo Kamanda Muliro

Thu, 16 Jun 2022 Chanzo: www.tanzaniaweb.live

Godbless Sawe, mkazi wa Kimara jijini Dar es Salaam, anatafutwa na Jeshi la Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam, kwa tuhuma za kumuua mkewe, Ester Benito Gadau, kwa kumkata kwa kitu chenye ncha kali kichwani, kisha kutokomea kusikojulikana.

Taarifa hiyo imetolewa leo Alhamisi, tarehe 16 Juni 2022 na Kamanda wa Polisi wa kanda hiyo, ACP Jumanne Muliro, akizungumza na wanahabari jijini Dar es Salaam. Kamanda Muliro amesema, mtuhumiwa alitekeleza tukio hilo tarehe 14 Juni 2022, maeneo ya Kibamba.

“Jeshi la Polisi Kanda Maalum ya Dar es salaam, linamtafuta Godbles Sawe, miaka 47, Mchaga, fundi Friji mkazi wa Kimara Suka, kwa tuhuma za kumuua mke wake Ester Benito Gadau, kwa kumkata kwa kitu chenye ncha kali kichwani huko maeneo ya Kibamba, Wilaya ya Ubungo na kukimbia baada ya kutekeleza mauaji hayo,” amesema Kamanda Muliro.

Katika hatua nyingine, Kamanda Muliro amesema, wamemfikisha mahakamani Joshua Simangwe, kwa tuhuma za kuwalawiti watoto watatu, ambao ni wanafunzi.

“Kesi kadhaa zimetolewa taarifa kwenye vituo vya Polisi, mkazo maalum umewekwa ili kesi hizi zipelelezwe haraka na baadhi ya watuhumiwa wamefikishwa mahakamani akiwemo Joshua Simangwe, miaka 66, mkazi wa Kipunguni Ukonga anayetuhumiwa kuwalawiti watoto watatu wenye umri chini ya miaka 18 ambao ni wanafunzi huko maeneo ya Gongolamboto Dar es salaam,” amesema Kamanda Muliro.

Chanzo: www.tanzaniaweb.live