Dar es Salaam. Watu wanne wamefikishwa katika Mahakama ya Wilaya Kinondoni, Dar es Salaam nchini Tanzania wakikabiliwa na shtaka moja la wizi wa pikipiki
Washitakiwa hao ni Juma Saidi (35), Abdallah Alifani (39), Ramadhani Selemani (39) na Rehema Abdalah (22).
Wakili wa Serikali Veronika Mtafya amedai jana Jumanne Julai 30, 2019 mbele ya Hakimu Lihamwike Boniphace kuwa Julai 8,2019 maeneo ya mikocheni Wilaya ya Kinondoni, Dar es Salaam washtakiwa hao waliiba pikipiki namba MC 237 yenye thamani ya Sh2,250,000 mali ya Elisha Bagarama.
Wakili Mtafya alidai washtakiwa hao kabla na baada ya kuiba walimtishia Ibrahimu Abdul, kwa kutumia bastola huku akisema upelelezi wa kesi hiyo haujakamilika na kuomba tarehe nyingine kwaajili ya kutajwa.
Naye wakili wa utetezi, Samweli Ntabalia aliomba upande wa mashitaka kukamilisha upelelezi mapema.
Baada ya maelezo hayo, Hakimu Lihamwike aliahirisha kesi hiyo hadi Agosti 13,2019 na washtakiwa wamepelekwa rumande kwa kuwa shitaka linalowakabili halina dhamana.
Pia Soma
- Hoteli iliyoshambuliwa na al-Shabab Kenya yafunguliwa
- Lowassa, Sumaye wakutana msibani
- MCT walaani kukamatwa kwa mwandishi wa habari