Kundi lingine la wahalifu 25 ambao wengi wao ni Vijana maarufu kwa jina la ‘Panya Road’ waliokamatwa wamefikishwa katika Mahakama ya Wilaya ya Ilala Kinyerezi Jijini Dar es Salaam kwa tuhuma za unyang'anyi wa kutumia silaha ikiwemo mapanga.
Watuhumiwa hao walifikishwa mbele ya Hakimu Mkazi wa Mahakama hiyo, Fadhili Luvinga kusomewa mashtaka sita yanayowakabili.
Waendesha Mashtaka, Mawakili wa Serikali Michael Ng'hoboko, Avelina Ombock na Nancy Mushumbusi walidai kuwa watuhumiwa kwa nyakati tofauti walitenda makosa hayo Aprili 24, 2022, Aprili 29, 2022 na Mei 25, 2022 na maeneo ya Gongo la Mboto, Kipunguni na Karakata Jijini Dar es Salaam.
Walidai watuhumiwa hao walifanya matukio kwa Wananchi mbalimbali kwa kutumia mapanga na kujeruhi kwa lengo la kupora mali.
Waendesha Mashtaka walidai upelelezi wa shauri hilo umekamilika na waliomba tarehe kwa ajili ya kusikiliza hoja za awali.
Watuhumiwa wote walikana mashtaka yao na kesi zao ziliahirishwa kwa tarehe tofauti ikiwemo 26/05/2022 na 30/05/2022 ambapo wamepelekwa rumande kutokana na makosa waliyoshtakiwa nayo hayana dhamana.