Dar es Salaam. Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) imemfikisha katika Mahakama ya Wilaya ya Ilala, ofisa forodha wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), Peter Mwangamilo kwa kushawishi rushwa ya Sh500,000.
Wakili wa Takukuru, Veronica Chimwanda leo Jumatatu Septemba 9, 2019 amedai mbele ya hakimu mfawidhi, Martha Mpaze kuwa mshtakiwa huyo alitenda kosa hilo Septemba 3, 2019.
Amedai siku ya tukio mshtakiwa alimshawishi Leonard Ruvumwa kutoa kiasi hicho cha fedha ili kurahisisha zoezi la uhakiki kwa kampuni ya kutoa na kupokea mizigo ya Maltlines International Tanzania.
Baada ya kusomewa shtaka hilo mshtakiwa alikana na upande wa mashtaka kudai upelelezi bado haujakamilika.
Hakimu Mpaze ametoa masharti ya dhamana, kumtaka mshtakiwa kuwa na mdhamini mmoja sharti ambalo lilitimizwa na mshtakiwa huyo.
Hakimu Mjaya ameahirisha kesi hiyo hadi Septemba 30, 2019 itakapotajwa tena.
Pia Soma
- Beki wa Manchester United atibiwa na "daktari wa miujiza" China
- Watumishi Wizara ya Kilimo wafikishwa mahakamani kwa madai ya kupokea rushwa
- Serikali ya Tanzania kubadilisha hadhi Pori Tengefu la Wembere