Morogoro. Jeshi la Polisi Mkoa wa Morogoro linamshikilia Luka Paulo (50) kwa tuhuma za ndugu wawili kufariki dunia wakiwa nyumbani kwake.
Imeelezwa kuwa mmoja wa ndugu hao alimpeleka mwenzake anayedaiwa kuwa ni mgonjwa wa akili kupatiwa matibabu kwa Paulo ambaye ni mganga wa kienyeji.
Akizungumza leo Jumanne Desemba 11, 2018 Kamanda wa polisi mkoani humo, Wilbroad Mutafungwa amesema ndugu hao walifariki Desemba Mosi, 2018 katika kitongoji cha Muheza wilayani Mvomero.
Mutafungwa amesema Lucian Epimark (54) maarufu kwa jina la Kigogo mkazi wa Chogoali aliyedai kuwa na matatizo ya akili alipelekwa na kaka yake, Gerald Epimark (60) kutibiwa kwa Paulo.
Amesema wakiwa wamelala nyumbani kwa mganga huyo, Lucian aliamka na kuanza kushambulia Gerald na kumpiga na tendegu la kitanda kichwani na kusababisha kifo chake.
Amesema baada ya tukio hilo Lucian naye alijinyonga kwa kutumia kamba.
Kamanda huyo amesema polisi wanamshikilia mganga huyo kwa ajili ya mahojiano.
Mutafugwa ametoa tahadhali kwa wananchi wanaoishi na watu wenye matatizo ya akili kuwapeleka hospitali, kuwashauri kuwa matatizo ya akili ni kama magonjwa mengine.
Amewataka waganga wa kienyeji kuacha kuwadanganya wananchi kuwa wana uwezo wa kutibu magonjwa ambayo yanapaswa kutibiwa hospitali.