Mzee mwenye umri wa miaka 71, Patrick Malya amehukumiwa kifungo cha miaka 20 jela baada ya kupatikana na hatia ya kusafirisha mirungi, akiwa ni mshtakiwa wa kwanza mwenye umri mkubwa kuhukumiwa kwa kosa la mirungi.
Adhabu hiyo imetolewa wakati Mkoa wa Kilimanjaro, hasa Wilaya za Rombo, Moshi, Hai na Mwanga zikitikiswa kwa biashara ya mirungi inayoingizwa kutoka nchi jirani ya Kenya, kupitia njia za panya zilizopo mpakani katika wilaya hizo.
Katika hukumu ya kesi hiyo, Jaji Emmaculate Banzi wa Mahakama Kuu Divisheni ya Makosa ya Rushwa na Uhujumu Uchumi iliyoketi Moshi, alimwachia huru mke wa mzee huyo, Paulina Mallya (60) kwa kukosekana ushahidi dhidi yake.