Dar es Salaam. Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu imemhukumu mwanasiasa Salma Mntambo kifungo cha miaka 99 jela, baada ya kupatikana na hatia katika mashtaka 17 ya kuwasilisha nyaraka za uongo na kujipatia fedha kwa njia ya udanganyifu.
Hata hivyo, miaka hiyo itakwenda sambamba hivyo atatumikia miaka sita jela. Mshtakiwa huyo aliyekuwa mgombea ubunge wa Korogwe Mjini mwaka 2015 kupitia ACT Wazalendo, alikuwa akikabiliwa na makosa 14 ya kujipatia fedha kwa njia ya udanganyifu na matatu ya kutoa nyaraka za uongo.
Akitoa hukumu hiyo jana, hakimu Kelvin Mhina alisema amepitia sababu za upande wa mashtaka na utetezi katika kesi hiyo hivyo katika makosa matatu ya kutoa nyaraka za uongo, mshtakiwa atatumikia kifungo cha miaka mitano jela kwa kila kosa.
Mhina alisema katika makosa 14 ya kujipatia fedha kwa njia ya udanganyifu, mshtakiwa atatumikia kifungo cha miaka sita jela kila kosa.
Hata hivyo, hakimu Mhina aliamuru mshtakiwa huyo kutumikia vifungo hivyo sambamba hivyo atakwenda jela miaka sita.
“Huo ndiyo uamuzi wa Mahakama lakini mna haki ya kukata rufaa, kuhusu suala la fidia nitatafakari na kufanya utafiti ili nije kutoa oda ambayo ni sahihi hivyo Oktoba 2 nitaitoa oda hiyo ya fidia,” alisema hakimu Mhina.
Pia Soma
- IGP Sirro mwenyekiti mpya shirikisho wakuu wa polisi Mashariki mwa Afrika
- Kenya kuzalisha umeme wa nyukilia
- Wakulima wataka Serikali ya Tanzania kuwalipa Sh36 bilioni
Katika kosa la kughushi, mshtakiwa Mntambo anadaiwa kati ya June mosi 2003 na Oktoba 31, 2011 maeneo yasiyojulikana wilayani Ilala, mkoani Dar es Salaam kwa nia ya udanganyifu alighushi risiti yenye namba 001226 ya Juni 10, 2003.
Anadaiwa alifanya hivyo kuonyesha kwamba Ridhuan Mringo alinunua nyumba ya Shirika la Nyumbala Taifa (NHC) iliyopo kitalu namba 710 mtaa wa Mfaume Upanga kwa Sh70 milioni akijua ni uongo.