Geita. Efrazia Maneno (22), mkazi wa kijiji cha Nyaseke kata ya Bulela mjini Geita nchini Tanzania anadaiwa kumuua kwa kumnyonga mwanae mwenye umri wa mwaka mmoja na miezi miwili kisha naye kujinyonga.
Tukio hilo limetokea jana Jumapili Agosti 18, 2019 saa saba mchana umbali wa mita 300 kutoka nyumba aliyokuwa akiishi, alitumia khanga kujinyonga katika mti wa mwembe.
Maneno Kapunda, baba mzazi wa Efrazia amedai binti yake alikua akiishi na babu na bibi baada ya wazazi kutengana na hakueleza tatizo lolote kabla ya kufanya uamuzi wa kujiua
“Huyu binti yangu alimaliza shule ya Sekondari Bulela akiwa mjamzito na mwanaume aliyempa mimba alikataa hivyo alibaki hapa nyumbani na wazee kwa kweli tukio hili limenishangaza,” amesema Kapunda
Ofisa mtendaji wa kijiji cha Nyaseke, John Maguta amethibitisha kutokea kwa tukio hilo na kusema polisi walifika jana jioni Jumapili na kutoa mwili uliokuwa ukining’inia na kuruhusu familia kuendelea na taratibu za mazishi yanayotarajiwa kufanyika leo Jumatatu kijijini hapo.
Jitihada za kumpata kamanda wa polisi mkoa wa Geita zinaendelea ili aweze kuzungumzia tukio hilo.
Pia Soma
- 29 wapandishwa kortini Morogoro tuhuma za uzembe, uzururaji
- Amchinja mkewe kisha kujinyonga
- Uchunguzi kujipiga risasi mwanafunzi Arusha unaendelea
“Hakuna uchunguzi unaofanyika maana mhusika mkuu amekufa na hata tukichunguza sio rahisi kupata ufumbuzi, “amesema Kisusi
Endelea kufuatilia Mwananchi kwa habari zaidi